JKCI Kutambulika Kimataifa kwa Kazi Bora za Upasuaji wa Moyo


Huduma bora za matibabu pamoja na upasuaji wa moyo zimeifanya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  kutambulika kimataifa na hivyo wataalamu wengi kutoka nje ya nchi kuvutiwa  kwenda kufanya kambi maalum za  matibabu  ya moyo kwa kushirikiana na madaktari wa Taasisi hiyo.

Hayo yamesemwa leo  na Mwakilishi wa Mufti,Sheik Hassan Said Chizenga wakati wa hafla fupi ya kuwashukuru wataalam wa afya kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia ambao wako JKCI  katika kambi maalum ya upasuaji wa moyo.
Sheik Chizenga alisema  Taasisi ya Moyo  imekua kimbilio kwa wagonjwa wa  Afrika na Dunia nzima kwa ujumla kutokana na huduma bora za matibabu ya moyo zinazolewa  kiufanisi.

“Taasisi hii imekua kioo si kwa Afrika tu bali Dunia nzima kwa kutoa huduma ya matibabu ya Afya ya moyo na upasuaji kwa wagonjwa ambao ni watanzania na wengine kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati” ,alisema Sheik Chizenga.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Agnes Kuhenga aliishukuru  nchi ya Saudi Arabia kwa ushirikiano inaouonyesha kwa Serikali ya Tanzania katika kuimarisha utaalam na kuboresha utoaji wa huduma za afya hapa nchini.

“Ushirikiano wa Tanzania na Saudi Arabia umelenga kuhakikisha watanzania wanakuwa na afya bora na kuweza  kushiriki katika shughuli mbalimbali  za kiuchumi na kulifanya taifa letu kufikia lengo la kuwa nchi ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025”, alisema Kuhenga.

Naye Naibu Balozi wa Saudi Arabia nchini, Mhe. Ahmed Al Ghamidi alisema katika kambi hiyo wataalamu kutoka nchi zote mbili wameweza kuunganisha nguvu na ujuzi waliokuwa nao na kufanya matibabu kwa wagonjwa.

Mhe.Balozi Ghamidi alisema, “Katika kambi hii ya siku saba maisha ya wagonjwa waliofanyiwa upasuaji yameweza kuokolewa na  pindi watakapopona watarudi nyumbani na kuendelea na majukumu yao ya kazi za kila siku”,.

Katika kambi hiyo jumla ya wagonjwa 20 wanatarajia kufanyiwa  upasuaji wa moyo wa kufungua kifua na kubadilishwa   valvu zaidi ya mbili ambapo hadi leo  wagonjwa 14 walishafanyiwa upasuaji na hali zao zinaendelea vizuri.
Mwakilishi wa Mufti Sheik Hassan Chizenga akimkabidhi tuzo ya kuthamini  utendaji kazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo  Agnes Kuhenga wakati wa hafla fupi ya kuwashukuru wataalam wa afya kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia walioko nchini kwa ajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa wagonjwa ambao valvu zao hazifanyi kazi vizuri. Kushoto ni Naibu Balozi wa Saudi Arabia Mhe. Ahmed Al Ghamidi.

Naibu Balozi wa Saudi Arabia Mhe. Ahmed Al Ghamidi  akimkabidhi zawadi Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Agnes Kuhenga wakati wa hafla fupi ya kuwashukuru wataalam wa afya kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini humo walioko nchini kwa ajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa wagonjwa ambao valvu zao hazifanyi kazi vizuri. Kushoto Mwakilishi wa Mufti Sheik Hassan Chizenga.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Agnes Kuhenga akimkabidhi tuzo ya kutambua kazi ya upasuaji wa moyo wanayoifanya kwa wagonjwa Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo pamoja na mishipa ya damu  Khalid Kamal Alhroub  kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia ambao wako JKCI kwa ajili ya  kambi maalum ya matibabu ya moyo. Hadi sasa jumla ya wagonjwa 14  wameshafanyiwa upasuaji wa moyo na kubadilishwa   valvu zaidi ya mbili.

Mwakilishi wa Mufti Sheik Hassan Chizenga akizungumza jambo na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji  wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Agnes Kuhenga wakati wa hafla fupi ya kuwashukuru wataalam wa afya kutoka Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia ambao wako JKCI katika kambi maalum ya matibabu ya moyo.

Mwakilishi wa Mufti Sheik Hassan Chizenga akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Balozi wa Saudi Arabia Mhe. Ahmed Al Ghamidi, viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete na wafanyakazi wa  Taasisi ya Kimataifa ya Kiislamu ya  Misaada (IIRO) ya nchini Saudi  Arabia mara baada ya kumalizika kwa hafla fupi ya kuwashukuru wataalam kutoka nchi hiyo ambao wako JKCI kwa ajili ya kutoa huduma ya  matibabu ya moyo.

Comments

Popular posts from this blog

JKCI yawafanyia upasuaji wa Moyo wagonjwa 36 bila kufungua kifua

Balozi wa Uholanzi nchini Mhe. Jeroen Verheul aipongeza Taasisi ya Moyo Nchini

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Shirika la Balsam Care & Care la nchini Saudi Arabia wakimfanyia mgonjwa upasuaji wa kuzibua mishipa ya moyo bila kufungua kifua

Katika kuadhimisha siku ya moyo Duniani tarehe 29/09/2018 Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Chama cha Madaktari wa Moyo Tanzania (THF) wafanya upimaji na utoaji wa elimu ya afya ya moyo bila malipo katika viwanja vya Hospitali ya Vijibweni iliyopo wilaya ya Kigamboni.