Balozi wa Uholanzi nchini Mhe. Jeroen Verheul aipongeza Taasisi ya Moyo Nchini
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imepongezwa
kwa jitihada zake inazozifanya za kuweza kuwafikia wananchi wengi kwa kutoa huduma bora za matibabu, elimu na
ushauri wa jinsi ya kuepukana na magonjwa ya moyo.
Pongezi hizo zimetolewa jana na Balozi wa
Uholanzi nchini Mhe. Jeroen Verheul alipokuwa akiongea na wafanyakazi wa Taasisi hiyo wakati
wa ziara yake ya kuangalia huduma mbalimbali za matibabu ya moyo zinazotolewa
kwa wagonjwa.
Mhe. Verheul alisema
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete ni moja ya Taasisi zinazofanya kazi vizuri ya
kutoa huduma ya matibabu ya moyo katika
nchi zilizopo Kusini mwa Afrika .
Kuhusu Ubalozi wake kushirikiana na Taasisi hiyo katika utoaji wa
huduma kwa wananchi alisema ataangalia ni jinsi gani watashirikiana katika programu mbalimbali za afya ambazo zinatolewa hapa nchini kupitia Ubalozi wa Uholanzi.
“Wiki tatu zijazo nitaenda nchini Uholanzi
ambako tuna mkutano wa mabalozi wote. Kupitia mkutano huo nitaangalia ni
Taasisi ipi ambayo itaweza kuja nchini kufanya matibabu ya moyo kama ilivyokuwa
kwa nchi zingine ambazo zinatuma wataalamu wake kuja katika Taasisi hii kutoa huduma za matibabu
kwa wananchi”,alisisitiza Mhe. Verheul.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa
Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi alimshukuru Mhe. Balozi kwa kuwatembelea na
kuona huduma mbalimbali wanazozitoa na
kusema kuwa wanajitahidi kuhakikisha kila mwananchi anayefika katika Taasisi
hiyo anapata huduma bora za matibabu ya moyo.
Alisema idadi ya wagonjwa wanaotibiwa katika
Taasisi hiyo imekuwa ikiongezeka kila mwaka ukilinganisha na miaka ya nyuma hii
inaonyesha kuwa hivi sasa wananchi wenye matatizo ya moyo wanaelewa ni wapi pa
kwenda kutibiwa magonjwa hayo.
“Kutokana na wataalamu wetu kuwa na utaalamu
wa kutosha na hospitali kuwa na vifaa vya kisasa tumeweza kufanya upasuaji kwa
wagonjwa wengi zaidi kwa mwaka 2018 ukilinganisha na mwaka 2017”.
“Mwaka 2018 tumefanya upasuaji wa kufungua
kifua kwa wagonjwa 1053 na bila kufungua kifua kwa wagonjwa 405 ambapo mwaka
2017 tulifanya upasuaji wa kufungua kifua kwa wagonjwa 225 na bila kufungua
kifua kwa wagonjwa 800”, alisema Prof. Janabi.
Akiwa katika Taasisi hiyo Mhe. Balozi Verheul alitembelea maabara
ya uchunguzi wa matatizo na tiba za magonjwa ya moyo (Cath Lab), jengo jipya la
watoto ambalo ukarabati wake ukikamilika litakuwa na
vitanda 32 na vitanda tisa katika chumba cha wagonjwa walioko katika uangalizi
maalum (ICU),
wodi ya watoto na wagonjwa waliofanyiwa na wanaosubiri kufanyiwa upasuaji wa
moyo wa kufungua kifua, chumba cha
upasuaji na chumba cha wagonjwa walioko katika uangalizi maalum (ICU).
Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi na Balozi wa Uholanzi nchini Mhe. Jeroen Verheul pamoja na wafanyakazi wa Taasisi hiyo wakiwa
katika picha ya pamoja mara baada ya kumaliza kwa ziara ya Mhe. Balozi ya kuona huduma mbalimbali za matibabu ya moyo
zinazotolewa kwa wananchi.
Comments
Post a Comment